Godbless Lema Augua Ghafla Gerezani, Ashindwa Kufika Mahakamani
Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema
Kesi iliyokuwa isikilizwe jana 21 Desemba 2016 inayomkabili Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema na mkewe, Neema Lema, wakituhumiwa kumtukana Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo, imeahirishwa kutokana na hali ya Godbless Lema kuwa mbaya gerezani.
Godbless Lema, Mbunge wa Arusha Mjini akiwa hospitali baada ya kuugua ghafla na kushindwa kufika mahakamani
Taarifa za Godbless Lema kushindwa kufika mahakamani zimetolewa na wakili wa serikali, Elizabeth Swai, kwa Hakimu Mfawidhi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi, Augustino Rwezile, ambapo alisema alipata taarifa kutoka kwa ofisa Magereza zikieleza kuwa mbunge huyo anaumwa na amepewa mapumziko hivyo asingeweza kufika mahakamani.
Godbless Lema akiwa na mke wake, Neema Lema.
Aidha, taarifa kutoka kwa kiongozi huyo wa Magereza hazikueleza wazi kuwa mbunge huyo anaugua ugonjwa gani.
Kuhusu kesi hiyo inayowakabili wanandoa hao wawili leo walikuwa wasomewe hoja za awali ambapo pia shahidi wa kwanza kutoka upande wa Jamhuri, George Katabazi, alikuwa atoe ushahidi.
Godbless Lema na Neema Lema wanakabiliwa na kesi ya kumtukana Mkuu wa Mkoa wa Arusha kitendo wanachodaiwa kuwa walikitenda kupitia ujumbe mfupi wa simu baada ya Rais Magufuli kumteua Mrisho Gambo kuuongoza mkoa huo.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi tarehe 18 Januari 2017.
Comments are closed.