Mpaka Home; Haya Ndo’ Maisha Halisi ya Darassa, Cheki Video Akipika Msosi Gheto
MAKALA YA MPAKA HOME: Na Imelda Mtema | Gaztei la Risasi Jumamosi, Toleo la Desemba 24, 2016
NIAJE mtu wangu! Sehemu pekee ya kujidai mimi na wewe ni hapa ambapo unapata fursa ya kuweza kujua maisha halisi ya mastaa wa Bongo, wengi wamezoea kuwaona mastaa wetu wakiwa katika uhusika kwenye kazi zao zilizowatambulisha kwa jamii lakini hapa tunakuletea upande wa pili wa maisha yao wakiwa majumbani.
Wiki hii safu hii iliibuka maeneo ya Makongo Juu (CCM), Kinondoni jijini Dar, nyumbani kwa mmiliki wa ‘wimbo wa taifa’, Muziki, Shariff Thabeet ‘Darassa’.
Msanii huyu anayetarajia kufanya bonge la shoo la ushindani dhidi yake na Ibrahimu Mussa ‘R.O.M.A’ kwenye mkesha wa Mwaka Mpya pale Dar Live, Mbagala Zakheem jijini Dar, ana mambo mengi anayofanya nje ya kazi yake na ili uweze kuyajua zaidi, twende pamoja hapa chini:
Mpaka Home: Nyumba imepoa sana jamani hakuna mdada wa kuichangamsha?
Darassa: (Kicheko) hapana hapa tupo ‘midume’ tu na wengine hawajaamka imechangamka tu.
Mpaka Home: Sasa kazi zote kama kupika na vitu vingine unafanya mwenyewe?
Darassa: Ndiyo, mbona hakuna kinachonishinda kama kupika, mimi mtaalamu pia siyo kwenye muziki tu, hata kama atakuwepo mpenzi wangu hapa naweza kumpikia na yeye amekaa maana suala la kupika siyo kwa mwanamke tu.
Mpaka Home: Sasa kama wifi yetu yupo kwa nini usimchukue jumla?
Darassa: Unajua kila kitu ni mpango kwa hiyo mambo yakienda sawa hakuna tatizo.
Mpaka Home: Tukiachana na kuhusu kupika vipi kuhusu kufua nguo zako na kupiga pasi , unapeleka kwa dobi au unafua mwenyewe maana wanaume wengi hawapendi hiyo kazi?
Darassa: Hizo kazi nafanya mwenyewe maana mimi sioni kama ni kazi kubwa kwa sababu nilikuwa nazifanya tangu kitambo.
Mpaka Home: Umebahatika kupata mtoto wa ujanani?
Darassa: Hapana ila namuomba Mungu anibariki katika hilo.
Mpaka Home: Ungependa mtoto wako afuate nyayo zako?
Darassa: Hapana namuacha awe huru kabisa achague kitu anachopenda mwenyewe.
Mpaka Home: Kuna tofauti gani katika maisha ya zamani na ya sasa kwa kipindi hiki nyimbo zako zimekuwa gumzo?
Darassa: Tofauti ni kubwa, sana kwanza kabisa maisha yangu yamebadilika kwa kiasi kikubwa kwa sababu huko nyuma nilikuwa nikiishi sehemu yenye vyumba vidogo lakini nashukuru sasa nipo sehemu kubwa na yenye mandhari nzuri na vitu vingi sana, sasa hivi vinaenda kirahisi.
Mpaka Home: Najua zamani ulikuwa unaweza kukaa hata kwa mama ntilie ukala ugali, hivi sasa unaweza kufanya hivyo?
Darassa: Kwa kipindi hiki inaweza kuwa ngumu lakini ugumu wenyewe unakuja kwa sababu unaweza kwenda kula kwa mama ntilie ikashindikana hata kula hicho chakula chenyewe maana watu wanaweza kukuzingira meza yote, lakini maisha hayo nayapenda sana maana mimi nimetokea hukohuko uswahilini.
Mpaka Home: Nini unachokipenda zaidi kwenye maisha yako?
Darassa: Napenda amani kuliko kitu chochote.
Mpaka Home: Nini unavutiwa nacho hapa nyumbani kwako?
Darassa: Navutiwa na chumba nilichokitenga maalumu kwa ajili ya viatu na kofia zangu.
Mpaka Home: Kwa nini?
Darassa: Unajua mimi tangu kitambo napenda sana viatu sasa zamani nilikuwa sina uwezo wa kuvinunua hivyo viatu vya shule ndiyo nilikuwa natumia kwa mitoko yangu pia, hivyo nilivyopata fursa ya kuweza hata kupata fedha ya kununua viatu nipendavyo hivi sasa ndiyo naitumia kukamilisha ndoto yangu.
Mpaka Home: Katika hilo unataka kuwaambia nini vijana wenzako?
Darassa: Nawaambia wataweza kutimiza ndoto zao kwa kujituma kwa nguvu bila kukata tamaa.
Mpaka Home: Hapa unapoishi ni nyumba yako umejenga au umepanga?
Darassa: Hapa nimepanga ila Mungu akipenda siku si nyingi nitakuwa na kwangu.
Mpaka Home: Kuna tetesi umetumia ndumba ndiyo maana nyimbo zako zimevuma kwa kasi ya ajabu?
Darassa: Hakuna kitu kama hicho, anayesema hivyo atakuwa tu ni mvivu wa kufikiria kwa sababu mimi nimehangaika kwenye hii ‘game’ karibu miaka kumi kwa nini nisingefanya kipindi hicho? Ni wakati wangu tu umefika.
Mpaka Home: Nakushukuru sana kaka yangu kwa ushirikiano wako.
Darassa: Karibu sana dada.
Comments are closed.