The House of Favourite Newspapers

Ishu ya Kuanzia Benchi, Makambo Afunguka

0

MSHAMBULIAJI wa Yanga, Heritier Makambo amefunguka kuwa hana tatizo lolote kwa yeye kuanzia nje huku mchezaji mwenzake, Fiston Mayele akianza kwa sababu kitu muhimu kwake ni kuona timu yao inapata ushindi bila kujali kuwa ameanza au yupo benchi.

 

Katika michezo miwili ya mwisho ya Yanga Makambo alianzia benchi na Mayele kuanza kikosi cha kwanza cha Kocha Nasreddine Nabi, ambapo michezo hiyo ni Ngao ya Jamii dhidi ya Simba na Ligi Kuu Bara dhidi ya Kagera Sugar.

 

Akizungumza na Championi Jumamosi, Makambo alisema kuwa licha ya yeye kuanza benchi lakini amefurahi kuona timu imepata matokeo mazuri kwani hicho ndio kitu cha muhimu kwake na timu kwa ujumla.

 

“Wala sifikirii kuhusu kukaa benchi na Mayele kuanza, muhimu kwangu ni timu kupata matokeo mazuri, unaona katika michezo ambayo sijaanza mimi timu ilipata ushindi hiyo inaonyesha kuwa wachezaji wote ni bora kila mmoja kwa nafasi yake na ukilinganisha na ukubwa wa Yanga.

 

“Najua kila mchezaji malengo yake ni kucheza katika kikosi cha kwanza lakini kila kitu mwalimu ndio anapanga lakini sina hofu na hilo kwa sababu ligi ndio kwanza inaanza,” alisema mchezaji huyo.

HAWA ABOUBAKHARI, Dar es Salaam

Leave A Reply