The House of Favourite Newspapers

Jinsi ya Kukabiliana na Matatizo Ya Ukeni

0

 

MATATIZO yanayotokea ukeni kitaalamu tunaita Vaginitis. Hali hii inaweza kusababishwa na maambukizi mbalimbali au isiwe inatokana na maambukizi bali ni mabadiliko ukeni. Ngozi laini ya ukeni iitwayo vaginal mucosa huathirika na wakati mwingine tatizo hupanda hadi nje ya uke.

Mwanamke mwenye tatizo hili hutokewa na dalili mbalimbali kama kutokwa na uchafu ukeni na muwasho, kuhisi moto kama pilipili ukeni, kujikuna sana na uke kuvimba. Tatizo hili la vaginitis pia ni miongoni mwa matatizo makubwa yaliyopo katika kundi la magonjwa sugu ya wanawake.

Hali kama hii inaweza kujitokeza na kuathiri nje ya uke peke yake na kuitwa ‘vulvitis’ na endapo itaathiri ndani na nje ya uke tunaita ‘vulvovaginitis’.

CHANZO CHA TATIZO

Tatizo hutofautiana ukali kutegemea na umri wa mwanamke. Makundi haya yanayopatwa na ugonjwa huu tunayagawa katika maeneo matatu, kwanza ni watoto wa kike ambao ni wadogo na hawajavunja ungo. Hawa hupata maambukizi toka katika bakteria wanaopatikana katika mfuko wa haja kubwa ambao hujipenyeza ukeni endapo huyu binti hatakuwa katika hali ya usafi sehemu zake za siri na wanaoathirika zaidi ni watoto wenye umri kati ya miaka miwili hadi sita.

 

 

Kiutaratibu mtoto wa kike baada ya kujisaidia haja kubwa asafishwe kwa kusukumia uchafu kuelekea nyuma siyo mbele. Epuka kumsafisha mtoto na sabauni kali katika maeneo yake ya ukeni. Watoto pia huweza kupata maambukizi mengine kama fangasi na bakteria.

 

Wanawake walio katika umri wa kuzaa pia huathirika sana na tatizo hili, hushambuliwa zaidi na maambukizi mchanganyiko yaani fangasi na bakteria, na wakati mwingine hupata maambukizi ya Trikomonia ambayo ni kutokana na ngono. Kwa kawaida, kwa mwanamke aliye katika umri wa kuzaa, bakteria aina ya Lactobacillus ndiyo walinzi wa uke na wakisumbuliwa tu kidogo, basi mwanamke atahangaika na tatizo la kutokwa na uchafu ukeni na muwasho mkali.

 

Lactobacillus kazi yao ni kuzalisha tindikali ukeni, kiwango cha tindikali ukeni ni 3.8 hadi 4.2, hii inasaidia kuzuia uzalishwaji wa aina nyingine ya vimelea vibaya ukeni. Uwepo wa vichocheo imara vya kike mwilini yaani homoni ya Estrogen husaidia kuimarisha afya ya uke na kinga dhidi ya maambukizi sehemu hiyo. Mambo yanayochangia kasi ya uke ushambuliwe na maambukizi ya mara kwa mara ni kupungua kwa kiwango cha tindikali ukeni. Tindikali au aside inapopungua ukeni husababisha alkali iwe juu. Alkali ikiwa juu huboresha mazingira yanayowafaa fangasi na bakteria. Tindikali hupungua ukeni pale mwanamke anapokaribia siku zake na ndiyo maana wanawake wengine hulalamika muwasho mkali na kutokwa na uchafu ukeni siku chache kabla ya hedhi.

 

Kipindi cha damu ya hedhi pia tindikali huwa chini na husababisha maumivu na muwasho ukeni wakati wa hedhi. Uwepo wa manii ukeni vilevile huchangia kupunguza tindikali, ndiyo maana baadhi ya wanawake hulalamika muwasho baada ya kujamiiana. Mwanamke kutokuwa msafi sehemu zake za siri na nguo zake za ndani pia ni mojawapo ya vyanzo vya tatizo hili. Kujisafisha sana ukeni pia huchangia tatizo hili.

 

Matumizi ya baadhi ya pedi nayo huweza kusababisha muwasho na kutokwa na uchafu. Wanawake wazee nao huathirika na tatizo hili kutokana na kupungukiwa na vichocheo vya Estrogen. Mwanamke aliyeondolewa vifuko vya mayai wakati wa upasuaji, wanawake wanaopigwa x-ray za kiuno au tumbo mara kwa mara, wanaotumia dawa za kansa nao wote hukumbwa na tatizo hili.

Kipimo cha Ultrasound hakina madhara na hapa hakihusiki kuleta madhara yoyote hata kikifanyika mara nyingi. Kwa hiyo mwanamke yeyote anaweza kupatwa na tatizo hili bila kujali umri wala taifa.

 

DALILI ZA UGONJWA

Kama tulivyoona hapo awali tatizo hili huambatana na kutoka uchafu ukeni ambao ni majimaji mepesi na huwa kama maziwa mtindi, husababisha ngozi ya ukeni iwe nyembamba na ina gamba. Uchafu huo unapotoka kwa nje ukeni hukauka na kuganda. Mwanamke hulalamika maumivu wakati wa kukojoa, maumivu wakati wa kujamiiana.

Hali hii humkosesha usingizi na kushindwa kulala na huhisi kupata nafuu anapojimwagia maji ya moto ukeni.

 

UCHUNGUZI NA TIBA

Hufanyika katika kliniki za magonjwa ya akina mama, vipimo mbalimbali vitafanyika kadiri daktari atakavyoona inafaa. Tatizo hili halihusiani na Yutiai kama ilivyozoeleka na watu wengi. Ni vizuri umuone daktari bingwa wa akina mama katika hospitali za mikoa vinginevyo utajikuta kila siku unatumia dawa bila kupona, unapata nafuu ya muda baadaye tatizo.

 

NA DK. CHALE | IJUMAA | AFYA
SIMU: +255713350084

Leave A Reply