Rais John Pombe Magufuli ‘JPM’
Na Oscar Ndauka, Risasi Jumamosi
DAR ES SALAAM: Kitendo cha Rais John Pombe Magufuli ‘JPM’ kutengua uteuzi wa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anne Kilango Malecela kabla ya kumaliza mwezi mmoja wa utumishi madarakani kumeibua jipya ambalo linafanana na tukio hilo, Risasi Jumamosi limechimba.
Anne Kilango aliyepoteza ubunge wa Jimbo la Same Mashariki (CCM) mkoani Kilimanjaro kwenye uchaguzi mkuu uliopita akiwa Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, ameshabihiana tukio na aliyewahi kuwa mbunge wa jimbo hilo mwaka 1980, Chediel Yohana Mgonja.
Mwaka 1982, Mgonja alipoteza ubunge wa Jimbo la Same akiwa Waziri wa Utamaduni Vijana na Michezo kufuatia Mahakama ya Rufaa kubatilisha ushindi wake mwaka 1980.
Anne Kilango Malecela
Rais wa Tanzania wakati huo, Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere alimteua Mgonja kuwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga lakini akatengua uteuzi huo kabla ya mwezi mmoja kumalizika.
Kwa upande wake, Anne Kilango naye alikuwa Mbunge wa Jimbo la Same na naibu waziri, akaanguka ubunge, Rais JPM akamteua kuwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga lakini akatengua uteuzi wake kabla ya mwezi mmoja.
Kwa Anne Kilango iko hivi
Wakati akiwaapisha wakuu wapya wa mikoa kwenye Ikulu ya Dar es Salaam, Machi 15, mwaka huu, mama Kilango akiwa mmoja wapo, Rais Magufuli aliwaagiza kwenda kupambana na watumishi hewa katika mikoa yao.
Aidha, rais aliwapa siku 15 kuhakikisha watumishi hewa wote wanabainika na ripoti zipelekwe kwake. Kilichomtokea mama Kilango ni kuzungumza na waandishi wa habari akisema kwa mujibu wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga (Ras), Abdul Rashid Dachi, mkoa huo hauna watumishi hewa.
Rais aliposikia taarifa hiyo alituma wapelelezi wake mkoani humo ambao walibaini watumishi hewa 45 waliokuwa wameshalipwa Sh. milioni 339.9, hivyo rais aliamua kutengua uteuzi wake kwa Anne Kilango akisema alikubali kudanganywa na Ras wake.
Kwa Mgonja ilikuwa hivi
Katika uchaguzi wa mwaka 1980, Mgonja alishitakiwa kwenye kesi ya uchaguzi kwa madai ya kuiba kura kwa hiyo ushindi wake wa ubunge ukabatilishwa kwa kuvuliwa ubunge.
Pia, Mahakama ya Rufaa ilimhukumu Mgonja kutoshiriki mambo ya siasa au uchaguzi wowote ule kwa miaka 10 tangu kubatilishwa kwa ushindi wake.
Mwalimu akamteua kuwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga kabla ya kumalizika adhabu yake. Mwanasheria Mkuu wa Serikali (wakati huo), Jaji Joseph Sinde Warioba alimshauri Waziri Mkuu, Edward Moringe Sokoine (wakati huo) kutengua uteuzi huo kwa vile ungeleta mgogoro wa kikatiba kwa mtu kupewa wadhifa akiwa kwenye adhabu, Sokoine naye alimshauri Mwalimu ambaye alitengua ndani ya siku chache tu.
Baadhi ya wasomaji waliotaka kuchambuliwa kwa kina kuwepo kwa kufanana kwa tukio hilo walihoji ‘mkosi’ upo wapi kati ya Jimbo la Same au Mkoa wa Shinyanga?!
“Yaani watu wa jimbo moja, wote waukose ubunge tena wakiwa mawaziri halafu wapewe ukuu wa mkoa huohuo halafu watenguliwe katika kipindi kifupi ni jambo la ajabu sana! Sijui wapi pana mkosi, Shinyanga au Same?” baadhi ya wasomaji walihoji swali hilo la kufanana.
Mgonja alifariki dunia Januari 30, 2009 kwa ugonjwa wa kisukari na shinikizo la damu jijini Dar.