MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, leo imesikiliza kesi ya Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi (TSNP), Abdul Nondo juu ya kupata dhamana na uwakilishi wa kisheria.
Nondo ambaye ni mwanafunzi wa mwaka wa tatu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Iringa leo.
Mahakama hiyo, imepanga Aprili 4, 2018 kusikiliza maombi hayo. Uamuzi huo umetolewa leo Machi 21, 2018 na Jaji Rehema Samuje wakati shauri hilo lilipofikishwa mahakamani hapo kwa ajili ya kutajwa.
Hatua hiyo inatokana na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC), Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) na Mtandao wa Wanafunzi Tanzania(TSNP) kuomba mambo matatu likiwemo la Nondo kupewa dhamana.
Jaji Sameja ameutaka upande wa Jamhuri kujibu hoja za utetezi dhidi ya Nondo, Machi 26, 2018.
“Kesi ya msingi itakuja kusikilizwa Aprili 4 lakini upande wa Jamhuri mnatakiwa kuja kujibu hoja za upande wa wawasilishaji maombi,” alisema Jaji Sameja na kuongeza: “Pia upande wa wawasilishaji maombi mnapaswa kuwasilisha maombi ya nyongeza Machi 27, mwaka huu.”
Machi 19, 2018 THRDC, LHRC na TSNP waliwasilisha maombi namba 49, 2018 Mahakama Kuu kutaka itoe amri kwa Jeshi la Polisi kumpeleka mahakamani Nondo.
Wakili wa Nondo, Jebra Kambole, amedai maombi hayo yalifunguliwa dhidi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambapo wapeleka maombi wanaiomba mahakama kutoa amri ya kuletwa mahakamani kwa mwanafunzi Nondo au kumuachia kwa dhamana kwani ameshikiliwa na polisi kwa muda mrefu bila sababu za msingi kutolewa.
Hata hivyo, kwa sasa Nondo amenyimwa dhamana na mahakama mjini Iringa ambayo inataka kujiridhisha na usalama wake.
HABARI: DENIS MTIMA /GPL
Comments are closed.