MASTAA WASHEREHEA BETHIDEI NA WATOTO YATIMA
PWANI: Mastaa mbalimbali wa filamu wakiongozwa na Ndumbangwe Mithayo ‘Thea’, Blandina Jagula ‘Johari’ na Chiki Mchoma, jana waliungana na mwigizaji mwenzao Luckness Mokiwa kusherehekea sikukuu ya kuzaliwa ya mwanaye aitwaye Tayana (2) wakiwa na watoto yatima.
Mastaa hao walifanya tukio hilo katika Kituo cha Watoto Yatima cha Buloma Foundation kilichopo maeneo ya Picha ya Ndege, Kibaha mkoani Pwani ambapo Luckness alisema tofauti na mwaka jana mwanaye huyo alipokuwa anatimiza mwaka mmoja, mwaka huu aliona amuandalie sherehe hiyo kwa staili tofauti.
“Nimeguswa kufanya bethidei ya mwanangu pamoja na watoto hawa ambao kwa namna moja au nyingine wanakosa furaha kama hii, kuwatembelea kama hivi na kula pamoja, kunawapa nguvu mpya ya kupigania ndoto zao,” alisema Luckness huku wasanii hao kila mmoja naye akipewa nafasi ya kuwatia moyo watoto hao.
Thea aliyenukuu vifungu mbalimbali vya Biblia, aliwafariji watoto hao kwa kuwasomea neno hilo la Mungu huku akiwataka wazidi kumuomba Yeye waweze kufikia malengo yao.
Kiongozi wa kituo hicho, Baraka Kyando, alimshukuru Luckness kwa zawadi mbalimbali alizozitoa pamoja na waalikwa wote waliohudhuria sherehe hiyo na kuwataka watu wote kujijengea desturi ya kutembelea kituo hicho na kuwatia moyo watoto hao.
“Unajua mnapokuja kama hivi mnaongeza nguvu ya ziada katika kuwashibisha watoto hawa waishi katika ndoto zao, hapa kuna watoto tumewapokea wakiwa wadogo, wapo wanaosoma shule ya msingi na wengine sekondari na mmoja yupo chuo,” alisema Kyando.
Kituo hicho kina jumla ya watoto yatima 37 ambapo kati yao, wa kiume ni 20.
Stori: Mwandishi Wetu.