The House of Favourite Newspapers

Mbelgiji Yanga: Nawataka Simba

0

SIKU

chache baada ya Mbelgiji, Luc Eymael kutua nchini kuja kuinoa Yanga, ametamba kwamba anataka sana kukutana na wapinzani wao wa jadi Simba kutokana na kutowaogopa hata
kidogo.

 

Mbelgiji huyo ameweka wazi kwamba hawaogopi hata kidogo Simba kutokana na kuwa na uzoefu wa kucheza mechi za derby ikiwemo kubwa ya DR Congo alipokuwa AS Vita wakicheza na TP Mazembe.

 

Kocha huyo alitua Alhamisi hii kwa ajili ya kuchukua mikoba ya Mkongomani,
Mwinyi Zahera ambaye alivunjiwa mkataba wake. Mbelgiji huyo ameliambia Spoti Xtra, kuwa:

 

“Kwanza ijulikane derby ni mechi ya kipekee lakini linapokuja suala la mpira basi ijulikane ni dakika 90 na mnapokuwa uwanjani wote mnakuwa na asilimia 50 ya kushinda.

 

“Lakini kocha ambaye amewahi kukutana na timu kama za Kaizer Chiefs na Orlando Pirates za Afrika Kusini anakuwaje na hofu na mechi ya derby?

 

“Mimi siwezi kuwa na presha na mechi za namna hiyo kwa sababu ndiyo nazipenda kwa sababu nimeshazicheza kubwa tu, wakati nipo AS Vita tulicheza na TP Mazembe.

 

“Lakini natambua hii ni derby kubwa kwa hapa Tanzania na naifananisha na timu kubwa Afrika kama Zamalek na Al Ahly.

 

“Pia nimewafuatilia Simba hata ile mechi ambayo tulikuwa nyuma kwa mabao mawili kisha tukarudisha yote, nadhani tulifanya kitu bora sana katika mechi ile.”

Wakati kocha huyo muda wowote akitarajiwa kusaini mkataba wa kuifundisha Yanga, Ofisa Mhamasishaji wa Yanga, Antonio Nugaz, alisema:

“Kwa sasa tunafuatilia vibali vya kocha na tunataka aanze kazi kwa kukaa katika benchi kwenye mechi ya ligi dhidi ya Kagera Sugar Jumatano ijayo.

 

“Mchakato unaendelea na tunaamini kabisa kabla ya mechi hiyo basi kila kitu kitakuwa kimepatikana na kocha atakuwa ameanza kazi rasmi.” Baadhi ya timu alizozifundisha Mbelgiji huyo ni AS Vita, AFC Leopards, Rayon Sports, AlNasr, Al-Merrikh, Polokwane City, Free State Stars na Black Leopards.

Leave A Reply