The House of Favourite Newspapers

Msuva awatolea povu Kichuya, Mbaraka

Musa Mateja | CHAMPIONI| Dar es Salaam

USHINDANI wa mbio za ubingwa wa Ligi Kuu Bara unaendelea kwa kasi lakini upande wa pili wale wanaowania ufungaji bora nao mambo yamenoga.

Kiungo mshambuliaji wa Yanga, Simon Msuva, ana mabao 12 na ndiye anayeongoza, anafuatiwa na Shiza Kichuya wa Simba na Mbaraka Yusuph wa Kagera Sugar wenye mabao 11 kila mmoja, sasa Msuva ametoa kauli juu ya wapinzani wake hao.

Msuva amedai kuwa hawamtishi kwani wote kwa pamoja wanafukuzia nafasi hiyo wakiwa wamejikusanyia mabao 11 nyuma yake, akiwa na mabao 12.

Akizungumza na Championi Ijumaa, Msuva alisema hatishiki na suala la ushindani wa mabao, kikubwa anamuomba Mungu amjalie asipate maumivu yoyote kwani akiwa salama atahakikisha anaitendea haki kila nafasi ya kufunga atakayoipata, maana aliye nyuma yake kwa mabao si Mbaraka Yusuph pekee kwani hata Kichuya naye yuko karibu yake akiwa na mabao 11, sawa na Mbaraka.

“Nina imani hii imeshakuwa changamoto, ila kwangu naamini siku zote katika maisha huwezi kupata kitu kirahisi pasipo kupambana kwa uwezo wote, naamini kila kitu kinawezekana hivyo nitamuomba Mungu anijalie ili maumivu yanipitie mbali tu, kwani nikiwa fiti hakika nitaonyesha maajabu.

“Siwaogopi wala hawanitishi kuwa karibu yangu, kwani kila jambo linawezekana ukilifanyia kazi vizuri ndani ya uwanja, hakika najiamini, uwezo wangu ni mzuri kuliko wao japo natambua nafasi kama hii huwa inaendana na bahati kubwa, suala la uwezo binafsi pia lina nafasi kubwa sana kwenye mpira, hivyo sitishiki na lolote,” alisema Msuva.

Comments are closed.