The House of Favourite Newspapers

Ndoa na Shetani-11

0

ILIPOISHIA:
“Jijini Nairobi tunakula vichwa, tena nimekumbuka itabidi twende wote achana na mawazo ya kurudi nyumbani, bado una nafasi ya kutengeneza pesa na kurudi nyumbani ukiwa vizuri heshima itakuwepo.”
SASA ENDELEA…

Mmh! Kweli eeeh,” nilijikuta nimeondoa mawazo ya kurudi nyumbani kinyonge bali kwenda kutafuta ili nirudi nikiwa vizuri, heshima iwepo. Kwa kauli ya shoga yangu Doi kama alivyopenda kujiita kwa kifupi jina lake kamili alikuwa Doto baada ya kuzaliwa mapacha.
Siku zote ukifunga ndoa na shetani yataka nguvu ya Mungu kuivunja, nilijikuta nabadili wazo la kwenda nyumbani kuomba msamaha kwa wazazi wangu.
Nilikubaliana na shoga yangu kubadili upepo kwa kwenda nchini Kenya kula vichwa niliamini kwa jinsi nilivyokuwa biashara yangu ingekuwa nzuri.
Safari ya kurudi nyumbani ilivunjika na kukubaliana tuishie Same alipokuwa akienda shoga yangu Doi kwa wazazi wake.
Ilikuwa tofauti na mimi mwenzangu yeye kwao walikuwa radhi naye kwa vile kila alichokichuma aliwapelekea kwao na kurudi kazini.
Tulipofika kwao tulipokelewa vizuri na kutambulishwa kwa wazazi wake kuwa tupo pamoja, tunafanya kazi Dar katika duka kubwa la kuuza bidhaa mbalimbali ‘Super Market’.
Wazazi ndugu na jamaa walinifurahia, maelezo ya shoga yangu yalionesha kabisa familia yake ilikuwa haijui kazi aliyokuwa akiifanya na kudanganya anafanya kazi za kuajiriwa na si kuuza mwili.
Tulipokutanisha macho aliniminya jicho nikae kimya.
Mwanzo maelezo yake yalinishtua lakini aliponiminya jicho nilijua wazazi wanauziwa mbuzi kwenye gunia hivyo nilikuwa mpole. Kwa kweli familia ya shoga yangu ilionesha upendo wa hali ya juu huku ikionekana kujawa na furaha baada ya kupotezana na mtoto wao kwa miaka miwili.
Tulikaa kwa wiki nzima kisha tuliaga na kuondoka huku wazazi wa shoga yangu wakituombea dua maisha yetu yawe yenye mafanikio, Mwenyezi Mungu atutangulie kwa kila jambo bila kujua biashara tunayokwenda kufanya haimpendezi Mungu lakini ilibakia siri yetu.

Kwa vile sikuwa na paspoti, Doi alinisaidia kupata ya muda mpakani, tulipitia njia ya Taveta. Tulifika Nairobi majira ya saa moja na nusu usiku na kwenda sehemu moja ya uswahilini iitwayo Kawangware.
Shoga yangu alikuwa akikaa na rafiki zake wawili waliokuwa wakikaa gheto moja. Ndani ya chumba kulikuwa na kitanda kimoja cha sita kwa sita, tivii, meza ya kawaida iliyokuwa na vipodozi, jiko la mafuta, vyombo vichache na nje kulikuwa na jiko la mkaa.
Tulipofika tuliwakuta shoga zake Doi wakijiandaa kwenda kazini kwa kuvaa nguo za nusu uchi. Nina imani tupo pamoja tangu mwanzo wa mkasa huu. Kazi haikuwa ya kuajiriwa bali ya kuuza mwili. Walipotuona walitupokea kwa furaha kuonesha wana maisha ya maelewano.
“Waooo shoga, za Tizedi?”
“Ziko poa, za hapa?”
“Hata za hapa ziko poa.”
“Naona mnaingia kwa kazi?”
“Yaap, vipi nawe unaingia au umechoka na safari?”
“Leo sitoki si mnaona nina mgeni, huyu ni ndugu yangu,” Doi alinitambulisha kwa shoga zake.
“Ooh! Mazee, karibu sana.”
“Asante.”
“Amekuja kutembea au?”
“Amekuja kwa kazi si mnamuona analipa?”
“Tena analipa ile mbaya.”
“Konso hawa ni ndugu zetu huyu anaitwa Sipe kifupi cha Sipesroza ni mwenyeji wetu lakini anatokea Gilgil.”
“Gilgil ndiyo wapi?”
“Ipo njia panda ya kutoka Nakuru na Nyahururu kuja Naivasha kama unakuja Nairobi.”
“Ooh! Nimefurahi kukufahamu.”
“Na huyu anaitwa Bahati ni mwenyeji wa Burundi wote tumekutana hapa tukitafuta maisha na kuwa kama ndugu.”
“Nimefurahi kuwafahamu ndugu zangu.”
Itaendelea katika Gazeti la Risasi Jumamosi.

Leave A Reply