TAMBWE AANZA ‘KUWAMISS’ MSUVA, NIYONZIMA
STRAIKA wa Yanga, Amissi Tambwe ameanza ‘kuwa-miss’ wachezaji wenzake wa zamani Haruna Niyonzima na Simon Msuva kwa kusema walikuwa wanatoa mchango mkubwa kikosini mwao hivyo atawakumbuka kwa muda mrefu.
Yanga imemruhusu Msuva akajiunge na Klabu ya Difaa Al Jadida inayoshiriki Ligi Kuu ya Morocco wakati Niyonzima aliyemaliza mkataba amejiunga na Simba.
Tambwe ameliambia Championi Jumamosi kuwa, Msuva na Niyonzima ndiyo waliokuwa wapishi wakubwa wa mabao aliyofunga Yanga tangu alipojiunga na timu hiyo msimu wa 2014/15 akitokea Simba.
“Nitawakumbuka sana Msuva na Niyonzima kwa mchango wao kwangu na kwa timu nzima, nawatakia maisha mema huko waendako lakini nitawakumbuka sana.
“Walikuwa wanajua kunitengezea nafasi za kufunga, ukiangalia mabao yangu mengi niliyofunga wao ndiyo walikuwa wapishi wakubwa,” alisema Tambwe.
Hata hivyo, Tambwe alisema anaamini wachezaji waliopo kikosini sasa wataendelea kufanya kazi ya kumtengenezea mabao na kuendeleza kasi yake ya ufungaji.
STORI: SWEETBERT LUKONGE | CHAMPIONI JUMAMOSI