Baada ya kuwekwa mahabusu kwa siku nne, Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA na Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu leo amefikishwa Mahakama ya Kisutu, Dar es Salaam na kusomewa mashtaka ya kutoa lugha ya uchochezi.
Akisomewa mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri leo Jumatatu, Julai 24, mahakama imeelezwa kuwa Lissu ametoa lugha ya uchochezi dhidi ya Serikali Julai 17 akiwa maeneo ya Ufipa, Kinondoni.
Imedaiwa kuwa maneno hayo yalikuwa na lengo ya kuleta chuki dhidi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Alipotakiwa kukubali ama kukataa makosa hayo na Hakimu Mashauri, Lissu amesema kusema kweli haijawahi kuwa kosa la jinai.
Kwa sasa upande wa mashtaka wameomba Lissu anyimwe dhamana na upande wa utetezi wanapinga hoja ambazo bado zinaendelea.
Mahakama ya Kisutu imemnyima dhamana Tundu Lissu, kesi imeahirishwa hadi Julai 27, 2017 itakapotolewa uamuzi.
Lissu alikamatwa, Alhamisi, Julai 20 mwaka huu, katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) wakati akijiandaa kuelekea Kigali, Rwanda kwenye kikao cha Chama cha Wanasheria cha Afrika Mashariki (EALS).
Siku iliyofuata (Ijumaa), taarifa zilieleza kuwa polisi walikwenda kupekua nyumbani kwake na kuchukua iPad na CD na baadaye alipelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali ili kupimwa mkojo ambapo inaelezwa kuwa alikataa kwa madai kuwa kosa alilokamatwa nalo la uchochezi haliendani na kipimo cha mkojo.
Lissu anawakilishwa na mawakili 20 wakati serikali inawakilishwa mawakili 5. Aidha mawakili wa serikali wameomba Lissu anyimwe dhamana kwa kuwa ana mashauri matano mahakamani hapo yenye kesi za uchochezi, hivyo wamesema akiachiwa huru anaweza kudhuriwa.
Mawakili wa Lissu wanapangua hoja hizo.
PICHA NA DENIS MTIMA | GPL
INSTALL GLOBAL PUBLISHERS APP sasa usipitwe na matukio
PAKUA HAPA==>GLOBAL PUBLISHERS APP