The House of Favourite Newspapers

Utata Mkubwa Tuzo za TFF, Figisu Zatajwa

0

USIKU wa jana Alhamisi, Oktoba 21, 2021 Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) lilitoa tuzo kwa wachezaji, wadau wa soka, makocha, timu zilizofanya vyema katika msimu uliopita wa 2020/2021.

 

Tuzo hizo zilihusisha mashindano yote kuanzia Ligi Kuu mpaka Kombe la Ligi, ikihusisha Ligi ya wanawake na Wanaume.

 

Lakini kuna baadhi ya vipengele ambavyo wapenzi, wadau na wafuatiliaji wa masuala ya soka nchini wameonekana kukosoa na kuona pengine labda kuna figisu katika utolewaji wake.

 

TUZO YA MCHEZAJI BORA LIGI KUU BARA

Hii imekwenda kwa nahodha wa Simba, John Raphael Bocco, lakini msimu uliopita ndani ya kikosi hicho kulikuwa na mtu anayeitwa Clatous Chotta Chama, ambaye kwa sasa ametimkia nchini Morocco.

 

Wengi wanaamini kiungo huyo wa Zambia alistahili kubeba tuzo hiyo kwa mchango mkubwa aliouonesha kwa mabingwa hao wa Ligi Kuu na Kombe la Ligi.

 

Chama amepika idadi kubwa ya magoli Simba (amefunga mabao 8 na asisti 18, hivyo amehusika katika mabao 26 ambayo hakuna mchezaji aliyemfikia) , pia amekua kiunganishi wa timu, timu ilicheza kumtegemea yeye, ubora wake uwanjani kila mmoja anakubali.

 

TUZO YA KOCHA BORA LIGI YA WANAWAKE YA SERENGETI LITE

Aliyeibuka mshindi ni Kocha wa Yanga Princes, Edna Lema, lakini Simba Queens walitwaa ubingwa Ligi ya wanawake bila kupoteza mchezo hata mmoja,cha kushangaza, Kocha wao Mussa Mgosi hajapewa tuzo ya kocha bora wa msimu wanawake. Tulitaka afanye nini Zaidi.

 

TUZO YA MCHEZAJI BORA WA KOMBE LA AZAM

Hapa kiungo wa Yanga, Feisal Salum “Fei Toto” ameibuka kidedea lakini walio wengi wanampa heshima ya tuzo hiyo aliyekua kiungo mshambuliaji wa Simba ambaye amejiunga klabu ya Al Ahly ya Misri, Louis Miqquissone.

 

Wengi wameheshimu sana alichokifanya Fei Toto kwenye kombe la FA, lakini TFF wamelalamikiwa kufumba macho kwa kutaka kuweka mzani sawa, Miquissone ameibiwa tuzo yake alikuwa na maajabu kuliko Fei Toto, Labda amenyongwa kwasababu hayupo nchini.

 

TUZO YA MHAMASISHAJI BORA

Hii ilikwenda kwa Nick Leonard, maarufu kwa jina la “Bongo Zozo” Muhamasishaji bora, kama Antonio Nugaz hakuwa katika kinyang’anyiro, tuzo haikustahili kuwa na mpinzani tena mshindi ni Haji Manara Mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni.

 

Takwimu za Bodi ya Ligi wiki chache zilizopita ilionesha Mashabiki wa Yanga ndio walioongoza kwa kuhudhuria viwanjani lakini cha ajabu Nugaz hata jina lake halikuwemo.

 

Mpinzani wake wa karibu, Haji Manara ndio aliepaswa kubeba tuzo ile kwa namna alivyokuwa akiwahamasihsa mashabiki wa Simba kuhudhuria viwanjani.

MCHEZAJI BORA CHIPUKIZI

Hapa napo kuna utata, wadau wanahoji Abdul Seleman ‘Sopu’ anayechezea Coastal Union ambaye amepewa tuzo hii sio chipukizi, tayari amecheza Ligi Kuu kwa Msimu wa nne,Simba, Ndanda na sasa Coastal hivyo sio mhezaji chipukizi tena bali ameshakuwa mkongwe kwenye ligi, lakini pia timu yake imenusurika kushuka daraja.

Wadau wanasema kwa nini tuzo hiyo asipewe Deogratius Judika (wa Biashara United) ambaye ameisaidia timu yake kumaliza nafasi ya nne na sasa inashiriki Kombe la Shirikisho Afrika.

Tukumbukepia kwamba, kwenye masuala ya tuzo huwezi kumridhisha kila mtu.

Leave A Reply