The House of Favourite Newspapers

Uzimaji wa simu feki na Dhana ya kupanga ni kuchagua -2

0

lenovo-s960-fake-factory-test-mode

Wiki iliyopita msomaji wetu aliamua kupasuaji jipu kuhusu mada ya uzimaji simu feki, mawazo yake tumeyaheshimu na leo anaendelea kutoa hoja yake, fuatana naye:

Ikumbukwe pia kuwa idadi kuwa ya Watanzania wanaotumia huduma za simu za mkononi imeongezeka miaka ya karibuni kwa sababu ya kupatikana kwa urahisi na bei nafuu kwa simu na vifaa vyake.

Ikiwa simu hizi zitazuiwa kwa kigezo cha kutokuwa halisi kwa sababu yoyote itakayotolewa na taasisi yetu ya umma (Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania), Watanzania wengi wanaotumia simu hizi watakosa huduma hii. Wengi ni watu maskini wasio na uwezo wa kununua simu orijino za bei mbaya. Kwao hii ni anasa kubwa mno ambayo labda wapanga sera hawaioni kwa sababu kwao milioni ni fedha ndogo.

fake-phone-5-1-e1312203165990Najua watakuja na hoja nyingi za kuhalalisha kuzima simu hizi feki baada ya hapa, ila tuangalie na mambo haya ya msingi. Tanzania inajiandaa kisera na kiutendaji kwenda kwenye nchi ya uchumi wa kati. Uchumi wa viwanda ambao wadau wake wakubwa ni watafiti na wajasiriamali.

Lakini tunaanzia wapi katika kuanzisha hivi viwanda? Tukichukua mfano wa China wanaotengeneza vitu mbalimbali vikiwamo simu za mkononi hadi mashine kubwa za kuchimba madini, hawa wengi ni garage based industries. Yaani viwanda vidogo vidogo vinavyoanzia uani kwa mtu au gereji.

Mtu anaanza kwa kutengeneza bidhaa anayoweza kutengeneza katika taaluma au utundu alionao na kuendelea kuwa kiwanda kikubwa kwa kuwezeshwa na nchi yake. Ikiwa hivyo ndivyo Mtanzania atakayeanzisha kutengeneza simu za mkononi kwenye gereji yake anapewa nafasi gani kwenye soko la nchini kwao?
Kwa kigezo cha uhalisi na feki, simu hii itakuwa feki, kwa mujibu wa ITU kwani haitakuwa na IMEI.
Basi ni vema kwa wapangaji na watekelezaji wa sera za maendeleo ya nchi kufikiri mara mbilimbili maazimio yanayotolewa na mashirika ya huko nje.

Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere hakuruhusu kiholela wageni kuja nchini kuchimba madini na hata alipoulizwa alisema yaachwe hadi Watanzania watakapokuwa na elimu na ujuzi wa kutosha kuchimba wao wenyewe.
Nakumbusha lengo la kuanzishwa kwa vile vyuo vya ufundi wakati ule wa Nyerere ni kupata mafundi, viliweza kuzalisha watu wenye mbinu mbalimbali zinazoenda kutatua matatizo ya Watanzania moja kwa moja.

Hao ndiyo tuliwaita mafundi katika fani za umeme, maji, useremala, mawasiliano na nyingine nyingi. Vyuo hivi kama Dar es Salaam Technical College (DIT) vimebadilishwa na kuwa vyuo vikuu kwa sasa.
Hivyo uzalishaji wake wa mafundi wa fani mbalimbali umebadilishwa mwelekeo. Hata kule Mbeya na Arusha ambako kulikuwa na vyuo hivi vya ufundi, kumebadilishwa na kuwa vyuo vikuu.

Hata mashirika mengine ya umma kama TTCL na Tanesco yalikuwa na vyuo vyao vya ufundi, sijui kama vipo na vinaendelea kutoa taaluma husika. Anayeandika makala haya anaujuzi wa kutengeneza simu ya mkononi.

Lakini simu hiyo inatengenezwa kwa vifaa vya kuunganisha kimoja kimoja, hivyo kuchukua nafasi kubwa na kutoleta mvuto kwa mtumiaji. Hivyo basi tusisahau kuwa Watanzania wanatakiwa kupewa nafasi ya kuvumbua na kutengeneza simu. Wakati huo ni sasa.
Bado nasisitiza juu ya athari za majibu mepesi kwa maswali ya msingi. Kupanga ni kuchagua.
Kwame Ibwe amejitambulisha kuwa ni msomaji wa gazeti hili aliyeamua kupasua jipu.

Leave A Reply