Wachimba Madini 10 Wafariki Baada ya Mgodi Kuanguka Sudan
Wachimba dhahabu wapatao 10 wamefariki katika ajali iliyotokea kaskazini mwa Sudan, na wengine zaidi ya 20 kujeruhiwa.
Vyombo vya habari nchini humo vimelaumu kuporomoka kwa mgodi huo wa dhahabu kutokana na matumizi ya mashine nzito.
Ajali katika migodi ya Sudan ambayo haina uthibiti si jambo geni. Miezi sita iliyopita watu 11 walifariki katika tukio sawa na hilo katika eneo moja la Sudan kaskazini, huku vifo vingine vikiripotiwa katika jimbo la Darfur magharibi na Kordofan kusini.
Zaidi ya watu milioni mbili wanaaminika kufanya kazi katika sekta ya uchimbaji wa madini nchini Sudan.