SERIKALI imesema mafuriko mabaya zaidi kutokea ndani ya miaka zaidi ya 30 nchini China yamesababisha vifo vya watu takriban 140, huku wengine milioni 38 wakiathirika na nyumba 28,000 zikiharibika.
Kwa mujibu wa Wizara ya Maji, mito 33 imefurika huku tahadhari ikitolewa kwenye jumla ya mito 433. Majimbo yaliyoathirika zaidi ni pamoja na Jiangxi, Hubei, Hunan, Anhui, Zhejiang, Jiangsu na Chongqing.
Rais Xi Jinping amezitaka mamlaka zilizopo kwenye maeneo yaliyoathirika kuchukua hatua zaidi ili kuwasaidia wananchi walioathirika na janga hilo. Mvua zimekuwa zikinyesha katika baadhi ya maeneo nchini humo tangu mwezi uliopita.
Hata hivyo, mamlaka zimewatoa hofu wananchi kwamba pamoja na mafuriko hayo hali haiwezi kuwa mbaya kama mafuriko makubwa yaliyokuwa na uharibifu mkubwa yaliyoikumba nchi hiyo mwaka 1998.
Al-Jazeera