Yanga Wafalme wa Mapozi. Angalia Picha 9.
MAKALA: CHAMPIONI| LIGI KUU BARA
LINAWEZA kuwa ni jambo dogo lakini lenye maana kubwa, miaka ya zamani suala la picha za timu kabla ya mchezo kuanza lilikuwa na umuhimu mkubwa kwa kuwa ilikuwa ni kumbukumbu kwa watu wengi.
Mpaka sasa utamaduni huo upo lakini kwa kiasi fulani umepungua kufuatiliwa na wengi kutokana na kukua kwa teknolojia.
Pamoja na hivyo, bado ni muhimu ndiyo maana ni kawaida kuona timu nyingi kubwa na ndogo zikipiga picha kabla ya mchezo kuanza.
Hapa nchini, Yanga ndiyo ambayo imeonekana kuufanyia kazi utamaduni huo kwani wamekuwa na staili nyingi za kupiga picha tofauti na timu nyingine ikiwemo Simba ambayo huwa inakuwa na staili chache na wakati mwingine linaonekana siyo jambo muhimu au kubwa kwao.
Ni nadra kwa Yanga kuweka staili moja mara mbili au tatu mfululizo katika mechi zao kwa kuwa wamekuwa na kawaida ya kubadili na kuonekana ni watu wanaofanyia kazi kile wanachokifanya kabla ya kufika eneo la tukio.
“Tunajua kabisa, picha hizo zinatumika kwenye vyombo vya habari mbalimbali, hivyo ni lazima tutengeneze mwonekano mzuri wa picha za kuvutia,” anasema winga wa Yanga, Simon Msuva alipozungumzia suala hilo, anaendelea kusema:
“Tunaamini kuwa, kama picha zikiwa nzuri na zenye mwonekano mzuri wa kuvutia, basi ni lazima itatumika kwenye gazeti au mitandao ya kijamii.
“Tunajua Yanga ni kati ya timu inayoongoza kuwa na staili nyingi za kupiga picha, pamoja na kushangilia pale timu yetu inapopata ushindi au ubingwa.
“Nikuhakikishie tu, tutaendelea kupiga picha nyingi zenye staili tofauti kwa lengo la kuwa tofauti na timu nyingine, kikubwa hasa tunataka kuwa tofauti na timu nyingine.”
Kuhusu wabunifu wa staili za upigaji picha, Msuva anasema: “Wabunifu ni mimi, Juma (Abdul) na Dida (Deogratius Munishi).
“Kama ikitokea mechi hii nimetoa mimi staili ya ukaaji, basi inayofuata anatoa Abdul na nyingine inayofuata anatoa Dida.
“Mara nyingi staili zetu huwa zinatokea hapo kwa hapo na siyo jambo ambalo tunajifunza mazoezini.”
Comments are closed.