The House of Favourite Newspapers

Zitto Amaliza Utata Sakata la Urais Lissu, Membe

0

KAULI aliyoitoa Zitto Kabwe, Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo leo Jumanne, Septemba 22, 2020, imemaliza utata kwamba, chama hicho hakina jinsi isIpokuwa kuungana na kuwa na mgombea mmoja wa urais.

 

“Kumtoa Magufuli (Rais Dkt. John Magufuli) kunahitaji maamuzi magumu na ya kishujaa kutoka kwa viongozi wa vyama vya upinzani. Bila ya kuunganisha nguvu, hatoki,” ni kauli ya Zitto aliyoitoa leo kwenye ukurasa wake wa twitter.

 

Zitto ametoa kauli hiyo ikiwa ni siku moja kupita baada ya ‘msuguano’ kuanza kuchipua ndani ya chama hicho pale Maalim Seif Sharif Hamad, mwenyekiti wa chama hicho kueleza msimamo wa chama hicho kumuunga mkono Tundu Lissu, mgombea urais wa Tanzania Bara kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

 

Kauli ya Maalim Seif ilipingwa na kauli ya Bernard Membe, mgombea urais wa chama hicho siku hiyohiyo pale aliposema, “Mimi ndiye niliyekabidhiwa Ilani ya chama hicho kuinadi kote nchini kwenye uchaguzi huu. Taarifa zinazosambaa kuwa tayari tumejiunga na Chadema katika ngazi ya Urais siyo za kweli.”

 

Hivi karibuni, Lissu akiwa Visiwani Zanzibar, alitangaza Chadema kumuunga mkono, Maalim Seif kwenye nafasi ya urais akisema, yeye na chama chake hawawezi kupinga harakati za muda mrefu za mwanasiasa huyo visiwani humo.

 

Kwa muda mrefu chama cha Chadema na ACT-Wazalendo vilitangaza kuwa, katika meza ya majadiliano juu ya ushirikiano katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 28, 2020, licha ya kwamba hadi sasa vyama hivyo havijaweka wazi maazimio ya majadiliano hayo.

 

Hata hivyo, mara kadhaa viongozi wa vyama hivyo vya upinzani wamenukuliwa na vyombo vya habari wakionyesha dhamira ya kuungana katika uchaguzi huo.

 

Septemba 7, 2020, wakati akitambulishwa kwa wanachama wa ACT-Wazalendo katika Ukumbi wa Mliman City, jijini Dar es Salaam, Membe alisema atakuwa tayari kumuunga mkono mgombea yeyote wa upinzani mwenye nguvu ili kuing’oa CCM madarakani.

 

Leave A Reply