The House of Favourite Newspapers

Lulu Atokwa Povu Bethidei Yake Kubuma

0
Elizabeth Michael ‘Lulu’, (kushoto) akiwa na baadhi ya ndugu zake.

Na  GLADNESS MALLYA| RISASI MCHANGANYIKO| HABARI

DAR ES SALAAM: Kweli utawala wa awamu ya tano kiboko! Tofauti na miaka iliyopita ambapo mastaa mbalimbali hufanya kufuru katika kusherehekea kumbukumbu ya siku zao za kuzaliwa, Jumapili iliyopita, ambayo ilikuwa ni bethidei ya staa wa filamu, Elizabeth Michael ‘Lulu’, lakini haikufanyika.

Chanzo makini kilipolidokeza Risasi Mchanganyiko juu ya kutofanyika kwa shughuli hiyo, liliwasiliana na muigizaji huyo, lakini katika hali ya kushangaza, alitoa povu (kufoka) mno, akitaka watu kuachana na habari zake, kwa vile haziwahusu. Kwa miaka kadhaa iliyopita, Lulu alidhimisha bethidei yake katika hoteli kubwa au kumbi zenye ‘akili’ zikiambatana na mbwembwe nyingi za ulaji na manywaji, lakini mwaka huu imekuwa kimya.

“Mwaka huu Lulu hajafanya sherehe kama ilivyozoeleka miaka mingine iliyopita, hapo ndiyo unajua kiukweli mambo yamebana awamu hii, hakuna fedha, bethidei yake imebuma, hakuna cha ukumbini wala nini, hapana chezea utawala wa Rais Dkt. John Magufuli, kila mtu ana nidhamu ya fedha,” kilisema chanzo hicho.

Ili kuujua ukweli, Risasi Mchanganyiko lilimtafuta kwa njia ya simu Lulu ili kumsikia anazungumziaje kuhusu siku yake hiyo kubwa maishani mwake.

Risasi: Haloo Lulu, gazeti la Risasi hapa, hongera kwa kuongeza mwaka mwingine kwenye maisha yako.

Lulu: Asante sana.

Risasi: Je, bethidei yako ulifanyia wapi maana mashabiki wako wanapenda kujua ilikuwaje?

Lulu: Hilo haliwahusu.

Risasi: Kuna habari kwamba mwaka huu hujafanya sherehe kwa sababu ya ukata, hili likoje?

Lulu: Kama nimefanya au sijafanya linawahusu nini, kwanza kuanzia leo msinipigie simu tena, yaani sitaki kabisa simu zenu.

Risasi: Sisi tulitaka tu kuujua ukweli kuhusu suala la kwamba ukata ndiyo umesababisha sherehe isifanyike.

Lulu akakata simu.

Hata hivyo, wakati Lulu akishindwa kufanya sherehe hizo Jumapili, jana yake, msanii wa Muziki wa Kizazi Kipya, Isabela Mpanda, alifanya bethidei yake katika Ukumbi wa Belinda uliopo Mbezi Beach.

 

Leave A Reply