The House of Favourite Newspapers

Bongo Fleva, Singeli Kutikisa Leo Dar Live

HATIMAYE! Baada ya kusubiriwa kwa hamu na mashabiki wengi wa Muziki wa Bongo Fleva na Singeli, lile tamasha la Bonsi limewadia ambapo leo Sikukuu ya Idd wakali kibao wanatarajiwa kushuka na kuporomosha burudani mwanzo mwisho ndani ya Uwanja wa Taifa wa Burudani, Dar Live uliopo Mbagala-Zakhem jijini Dar.

 

WATOTO

Akizungumza na Over Ze Weekend, Mratibu wa Dar Live, Rajabu Mteta ‘KP Mjomba’ alisema pazia la burudani litafunguliwa mapema kuanzia saa mbili za asubuhi kwa ajili ya burudani kwa watoto.

“Kama ilivyo sikukuu zote watoto hufurahia ndani ya Dar Live na safari hii michezo imeboreshwa zaidi sambamba na burudani za hapa na pale za kumfanya mtoto ajisikie yupo kama ulaya vile.

 

“Tutakuwa na michezo ya kuogelea, kushindana kuimba na kucheza, kuvuta kamba bila kusahau kucheza na baiskeli buree ndani huku kwa wale watoto wenye ndoto ya kuendesha ndege wakipata nafasi ya kuingia na kukaa kwenye ndege ya kisasa,” alisema KP na kuongeza kuwa burudani hiyo itaenda kwa kiingilio cha buku 3 tu yaani 3,000.

Bonsi haina kulala

KP alisema burudani kwa watoto itahitimishwa saa 12:00 jioni na kufunguliwa rasmi burudani ya kiutu uzima ambapo tamasha rasmi la Bonsi litafunguliwa.

“Hili ni tamasha maalum kwa watu wa Bongo Fleva na Singeli na ndiyo maana linaitwa Bonsi. Kwa hiyo tutakuwa na wakali kibao wa Singeli kama Mzee wa Bwax, Easy Man ambao wataliamsha mwanzo mwisho huku mkali wa kupuliza matarumbeta, Kiroboto OG akifanya yake na kundi lake yaani usiku huu tarumbeta zitagongwa live jukwaani,” alisema KP.

 

WAKONGWE NDANI

Mbali na uwepo wa Singeli, jukwaa litatawaliwa na wakongwe kunako Bongo Fleva, Chid Benz na Mr Blue.

 

“Unapozungumzia wakongwe wanaojua kuliamsha jukwaani, huwezi kuacha kumtaja Chid Benz na Mr Blue, jamaa wanajua balaa na kuonesha hilo Mr Blue atapanda kuliamsha na ngoma zake zote hatari kuanzia za zamani hadi mpya huku Chid akiwamaliza kwa Dar es Salaam Stand Up.”

 

MOBETO KUMALIZA KILA KITU

Shoo haitaishia hapo kwani kwa mara ya kwanza katika muziki na ndani ya Dar Live, mwanamitindo, muuza nyago na msanii wa Bongo Fleva, Hamisa Mobeto atapanda jukwaa la Dar Live na kupiga ngoma zake zote kali.

 

“Wote tunajua Mobeto anavyokubalika kwa sasa, kwa hiyo tutegemee kuisimamisha Dar kwa muda ambapo atapiga ngoma zake zote kuanzia Tunaendana, My Love na Sawa,” alimaliza kusema KP. Kiingilio katika tamasha hilo kitakuwa shilingi 5,000 tu.

 

Comments are closed.