The House of Favourite Newspapers

Maafa Tanga: Watoto 5 Wafariki kwa Mafuriko

WATOTO watano wamekufa maji kutokana na mafuriko wilayani Korogwe mkoani Tanga na kufikisha idadi ya waliofariki kufikia 12 mkoani hapa kutokana na mvua.

 

Aidha, kaya zaidi ya 300 zimekosa makazi kutokana na mvua hizo zinazoendelea kunyesha kwa takribani wiki mbili sasa katika maeneo mbalimbali ya mkoani Tanga.

 

Pia daraja la Mto Mandera lililopo Kata ya Segera mpakani mwa Wilaya za Handeni na Korogwe mkoani Tanga limekata mawasiliano ya barabara kati ya mikoa mitano ya Tanga, Dar e Salaam, Arusha, Pwani na Manyara na kusababisha magari zaidi ya 200 kukwama kwa zaidi ya saa 36, huku abiria takribani 800 wakilala nje.

 

Mkuu wa Wilaya ya Korogwe, Kissa Gwakisa, alisema mafuriko hayo yametokea katika Kitongoji cha Magunga – Mzia Kata ya Foroforo baada ya nyumba iliyokuwa na watu wanane wa familia moja nyumba yao kuanguka nawatoto watano kati yao kusombwa na maji ambapo kati yao miili yote mitano imepatikana.

 

Kufuatia hali hiyo, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Korogwe ilifika katika kijiji hicho pamoja na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ambapo kwa kushirikiana na wananchi wamefanikiwa kufukua miili ya watoto hao iliyofunikwa na mchanga usiku wa kuamkia jana.

 

Gwakisa alisema watu 120 ambao makazi yao yamezingirwa na maji wamehifadhiwa katika kambi maalum kijijini hapo, na ametoa tamko la watu kutokurudi katika makazi yao hadi tamko la serikali hata kama hali itarejea kuwa ya kawaida.

Comments are closed.